MABADILIKO YA SIKU ZA IBADA SURA YA 1

SURA YA 1
BADILIKO KATIKA UTUNZAJI WA SIKU YA SABA
Mahali fulani katika zama za giza katikati ya siku zile za Kristo na siku zetu, utunzaji wa Sabato umebadilishwa kutoka siku ya saba ya juma kwenda siku ya kwanza.
Ni hakika ya kwamba amri ya Mungu inahusu kuitakasa na kuitunza siku ya saba kama Sabato. Hakuna uwezekano wowote wa kukosa kuelewa maana yake hapa. Amri ni hii:
"Ikumbuke siku ya Sabato uitakase. Siku sita fanya kazi, utende mambo yako yote; lakini siku ya saba ni sabato ya BWANA, Mungu wako, siku hiyo usifanye kazi yo yote, wewe, wala mwana wako, wala binti yako, wala mtumwa wako, wala mjakazi wako, wala mnyama wako wa kufuga, wala mgeni aliye ndani ya malango yako. Maana, kwa siku sita BWANA alifanya mbingu, na nchi, na bahari, na vyote vilivyomo, akastarehe siku ya saba; kwa hiyo BWANA akaibarikia siku ya sabato akaitakasa." (Kutoka 20:8-11).
Pia ni hakika kwamba hakuna amri nyingine yo yote iliyotolewa katika Maandiko Matakatifu inayoitaja siku nyingine au siku iliyo tofauti na hii. Biblia, katika utimilifu wake wote, yaani, Agano la Kale na Agano Jipya, inaamuru, inathibitisha, inatetea, na kufundisha utunzaji wa siku ya saba kama Sabato.  Vivyo hivyo ni kama ilivyo hakika kwamba makanisa mbalimbali yenye waumini Wakristo leo hii katika kila sehemu ya ulimwengu huu, ukiacha tofauti chache mno zilizo za muhimu, wanaitunza siku ya kwanza ya juma kwa pamoja, nao wanajiunga pamoja katika kuutetea utunzaji wake.
Basi, inaonekana ya kwamba kuna dosari kati ya uzoefu wa siku hizi wa makanisa mengi katika suala hili la utunzaji  wa Sabato na yale mafundisho yaliyo wazi kabisa ya Biblia.
Dosari hii inayoonekana wazi imeyasumbua mawazo ya wengi, na kufanya iwepo haja halisi ya kupata maelezo sahihi na yanayoaminika juu ya historia ya nyuma inayohusu badiliko hili katika utunzaji wa Sabato, wakati gani badiliko hili lilitokea, na sababu za kufanya badiliko hili. Kwa hiyo itatupasa kutafakari kwa makini maelezo ya Biblia yahusuyo kuanzishwa kwa Sabato miongoni mwa wanadamu, na sababu zitokanazo na fikara zake Mungu kwa kuamuru itunzwe katika mojawapo ya amri zake kumi.

SHERIA ILINENWA NA KUANDIKWA NA YEHOVA
Sheria pekee ya Mungu inayojulikana miongoni mwa wanadamu iliyoagiza utunzaji wa Sabato inapatikana katika Biblia, nayo imekwisha kudondolewa katika ukurasa huu. Ingetupasa kuonyesha wazi ya kwamba amri hii ilinenwa, pamoja na amri zile nyingine tisa, kwa kinywa chake Yehova Mwenyewe.
"BWANA [YEHOVA]  akasema nanyi kutoka kati ya moto; mkasikia sauti ya maneno, lakini hamkuona umbo lo lote;  sauti tu.  Akawahubiri agano lake, alilowaamuru kulitenda, yaani, zile amri kumi;  akaziandika juu ya mbao mbili za mawe." (Kumb 4:12,13).
Amri hizi kumi, ikiwamo amri hii ya Sabato, ziliandikwa kwa kidole cha Mungu Mwenyewe juu ya jiwe la kudumu. "Akaziandika juu ya mbao mbili za mawe." (Kumb 4:13). "Mbao mbili za ushuhuda, mbao mbili za mawe, zilizoandikwa kwa chanda [kidole] cha Mungu." (Kutoka 31:18).
Sheria hii inasemwa katika Maandiko kuwa ni "ya haki," "ya kweli," "nzuri," na "kamilifu." "Tena ulishuka juu ya mlima Sinai, ukasema nao toka mbinguni, ukawapa hukumu za haki, na sheria za kweli, na amri nzuri na maagizo." (Nehemia 9:l3).
"Sheria ya BWANA ni kamilifu" (Zaburi l9:7).Sheria hii inao wajibu wote umpasao mwanadamu.

KRISTO HAKUBADILI SHERIA
Halikuwa kusudi lake Kristo kubadili, kuondoa, kutangua, wala kuibatilisha sehemu yo yote ya sheria hii. "Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza."  (Mathayo 5:l7).
Badala ya kuitolea sheria hiyo sifa mbaya, Kristo alikuja kuifanya iadhimishwe.  "BWANA akapendezwa kwa ajili ya haki yake, kuitukuza sheria na kuiadhimisha." (Isaya 42:21). Naam, kwa kadiri Sabato inavyohusika, Kristo aliitunza, pamoja na kila amri nyingineyo.
"Siku ya sabato akaingia katika sinagogi kama ilivyokuwa desturi yake." (Luka4:16). Kusema kweli, imani kwa Kristo, badala ya kuiweka sheria kando, inaithibitisha na kuiimarisha. "Basi, je!  twaibatilisha sheria kwa imani hiyo?  Hasha! kinyume cha hayo twaithibitisha sheria." (Rum 3:31).
Sheria hii ya Mungu, ambayo ndani yake imo amri ya Sabato, inatangazwa na Paulo kuwa ni "ya rohoni," "takatifu," "ya haki,"  na "njema." "12Kwa maana twajua ya kuwa torati [sheria] asili yake ni ya rohoni." 14Basi torati [sheria] ni takatifu, na ile amri ni takatifu, na ya haki, na njema." (Rum 7:12,14).
Sheria hii ni lazima ishikwe kama sharti la kupata uzima wa milele. "Heri wale wazishikao amri zake, wawe na haki kuuendea huo mti wa uzima, na kuingia mjini kwa milango yake." (Ufu 22:l4, Tafsiriya King James Version).
Naam, hiyo ndiyo kanuni, au kipimo, ambayo  kwayo ulimwengu wote utahukumiwa. "Semeni ninyi, na kutenda kama watu watakaohukumiwa kwa sheria ya uhuru."  (Yakobo 2:12).
.
 SHERIA BADO INA NGUVU
Kwa hiyo, linaonekana kuwa ni jambo la ajabu kwamba utunzaji kama huo wa Sabato ungekuwa umebadilishwa hata kidogo.  Sheria hii ya Mungu bado ina nguvu.  Sheria hii inaamrisha utunzaji wa siku ya saba ya juma.  Lakini siku  hiyo haitunzwi hivi sasa na watu wengi mno wanaokiri ya kwamba wao ni watu wa Mungu.
Hata hivyo, sheria hii haibadiliki, bado ina nguvu, na hiyo ndiyo kipimo cha hukumu yake Mungu. Siku nyingine imewekwa badala ya siku iliyoamriwa.  Siku hiyo ilitoka wapi? Kwa nini imewekwa badala ya ile  iliyokuwapo?  Je, utunzaji wa siku hii [nyingine] unakubalika na Mungu? Haya ndiyo maswali ambayo sasa sisitutayashughulikia.

Ahsante na Mungu akibariki

No comments:

Post a Comment