CHANZO CHA IBADA ZA MAWIO YA JUA




Ibada za maawio ya jua zimetajwa katika Biblia. Lakini kile ambacho Mungu anasema kuhusu desturi hii si kile unachotarajia. Angalia mafungu haya ya kushangaza. Nabii Ezekieli alikuwa akionyeshwa, katika njozi, unabii wa muhimu juu ya dhambi za watu wa Mungu katika wakati wetu.
Muktadha mzima wa mafungu haya unahitaji kuchunguzwa kwa uangalifu ili kuelewa laana kuu ambayo Mungu anaijenga kuelekea kwenye hitimisho Lake:
Hebu turejee kitabu cha Ezekiel, tuone unabii kuhusu mambo haya tunayoyaangalia;
 “…Utaona tena machukizo makubwa mengine wanayoyatenda…na tazama, wanawake wameketi wakimlilia Tamuzi…Akanileta mpaka ua wa ndani wa nyumba ya Bwana, na tazama, mlangoni pa hekalu la Bwana, kati ya ukumbi na madhabahu, walikuwako watu kama ishirini na watano, wamelipa kisogo hekalu la Bwana, na nyuso zao zimeelekea upande wa mashariki, nao wanaliabudu jua, kwa kuuelekea upande wa mashariki. Basi, akaniambia, Umeyaona haya, Ee mwanadamu? Je! Ni jambo dogo…wayafanye machukizo wanayoyafanya hapa? Kwa maana…wamerejea nyuma ili kunikasirisha…Kwa sababu hiyo mimi nami nitatenda kwa ghadhabu; jicho langu halitaachilia, wala sitaona huruma, na wajapolia masikioni mwangu kwa sauti kuu, sitawasikiliza.” (Ezek. 8:13-18)
Kushika ibada za maawio ya jua ni jambo kubwa kwa Mungu! Anachukia sana kitendo hiki kiovu kiasi kwamba hatimaye atawaangamiza kabisa wale wote wanaodumu kuzifanya (Ezek. 9)!
Si “jambo dogo” kwa Mungu kwamba mamilioni wengi wanayafanya haya kila Isita! Inaweza kuonekana “maridadi,” “jambo la kidini”, na “linalogusa sana” kwa wale wanaolishiriki, lakini Mungu amewakataza watu wake wa kweli kubuni kawaida na fikira zao za kidini. Hapendezwi katika kile ambacho watu wanaweza kujisikia au kufikiri ni sahihi wao binafsi. Anapendezwa na wale ambao wanajali kile anachokifikiria! Kulingana na Mungu, ibada ya jua ya kale, iliyovishwa vazi zuri na kofia za Isita, ni namna ya ufungashaji wa kisasa wa desturi ya zamani sana, ambayo ni ibada ya sanamu ya kipagani.
Fikiria maneno ya Mungu mwenyewe katika Kumbukumbu la Torati 12:28-32:
“Maneno haya nikuagizayo yote yatunze na kuyasikiza...Bwana, Mungu wako, atakapoyakatilia mbali… nawe…kuketi katika nchi yao; ujiangalie, usije ukanaswa ukawafuata… wala usije ukauliza habari za miungu yao, ukisema, ‘Mataifa haya waitumikiaje miungu yao? Nami nifanye vivyo.’ Usimtende kama haya Bwana, Mungu wako; kwani kila yaliyo machukizo kwa Bwana, ayachukiayo yeye, wameifanyia miungu yao...Neno niwaagizalo lo lote liangalieni kulifanya; usiliongeze, wala usilipunguze.
Mungu huwaambia Wakristo wasichanganye kilicho cha uungu na kilicho cha kipagani—au ukweli na uongo! Usikubali watu wakuambie kwamba kile asemacho Mungu hakifanyi tofauti. Kinafanya!
Maandazi ya Moto Yenye Alama ya Msalaba
Nilipokuwa katika darasa la kwanza, watoto wote katika darasa langu walipaswa kila mmoja kuimba wimbo wa peke yake aliouchagua. Sitaweza kusahau wakati huu wa kutisha. Nilijisikia aibu sana kiasi kwamba nilichagua ule wimbo mfupi kabisa kutoka kwenye kitabu chetu kidogo cha nyimbo, “Maandazi ya Moto Yenye Alama ya Msalaba,” na kuuimba mbele ya darasa. Kwa kweli sikuwa na wazo la nini nilichokuwa ninaimba. Japokuwa ulikuwa mfupi (ulikuwa na maneno kumi-na-tano tu), sijaweza kusahau funzo la maana yake.
Angalia Yeremia 7:18: “Watoto huokota kuni, na baba zao huwasha moto, na wanawake hukanda unga, ili kumfanyizia mikate malkia wa mbinguni, na kuwamiminia miungu mingine sadaka za kinywaji, wapate kunikasirisha mimi.” Mikate iliyokuwa inatolewa kwa malkia wa mbinguni ilikuwa ni haya haya maandazi ya moto yenye alama ya msalaba ambayo mamilioni ya watoto leo huimba juu yake (Alexander Hislop, Babeli Mbili, uk. 107). Kile kinachoonekana kutokuwa na hatia si safi hata kidogo.
“Malkia wa mbinguni” ni nani?
Ashtorethi—Malkia wa Mbinguni
Ibada ya Asitate (Isita) daima iliambatana na ibada ya Baali au kuabudu jua. Asitate alikuwa mke wa Baali. Angalia kwamba jina lingine la Asitate lilikuwa ni Ashtorethi. Nukuu ifuatayo inaliweka hili wazi. “Neno Isita lenyewe lina maana gani? Si jina la Kikristo. Linabeba asili yake ya Kikaldayo kwenye paji lake la uso. Isita halina maana nyingine zaidi ya Asitate, moja ya cheo cha Beltisi, malkia wa mbinguni…Sasa, mungu mke wa Waashuru, au Asitate, anatambulishwa kuwa ni Semiramisi na Athenagorasi (Legatio, kit. ii. uk. 179), na Lucian (De Dea Syria, kit. iii. uk. 382)…Sasa, hakuna jina ambalo lingeweza kuonyesha tabia halisi ya Semiramisi, kama malkia wa Babeli, zaidi ya jina la ‘Asht-tart,’ kwani hilo maana yake ni “Mwanamke aliyejenga minara”…Basi, Ashturit…ni wazi kwamba ndilo hilo hilo la Kiebrania ‘Ashtorethi’” (Alexander Hislop, Babeli Mbili, ku. 103, 307-308).
Angalia nukuu hii hitimishi kutoka Ensaiklopidia ya Microsoft Encarta Multimedia: “Ishita alikuwa Mama Mkuu, mungu mke wa uzazi na MALKIA WA MBINGUNI.” Hivyo, kiuhakika, Ashtorethi (Ishita) alikuwa mjane kahaba mama/mke wa Nimrodi, Semiramisi, kama wengi wa wanahistoria wa kale wanavyoshuhudia! Sasa Isita imewekwa imara kwamba si kitu kingine zaidi ya Ashtorethi wa Biblia! Sasa tunaweza kuchunguza maandiko yanayoonyesha jinsi Mungu anavyoitazama ibada ya huyu mungu mke wa kipagani—kwa jina lolote!
Mungu Huiita Isita Uovu
Sasa kwa kuwa tunajua kuwa Isita ni mungu mke Ashtorethi, tunahitaji kutazama kwenye Biblia na kuona kile Mungu anachofikiria. Angalia fungu hili: “Wana wa Israeli walifanya yaliyokuwa ni maovu mbele za macho ya Bwana...Wakamwacha Bwana, wakamtumikia Baali na Maashtorethi [Isita]” (Amz. 2:11, 13).
Muktadha unaonyesha kwamba Mungu aliruhusu watu Wake wachukuliwe kutoka kwenye
nchi yao kwenda matekani kama matokeo ya dhambi hii! Huendelea, ikielezea jinsi ambavyo Mungu aliwakomboa watu Wake mara kwa mara tena kwa njia ya waamuzi. Baada ya kila ukombozi, Israeli aliwarudia miungu hao hao wa uongo, kitendo ambacho kilileta utekwaji nyara mara nyingine, kwa kushindwa na mataifa yaliyokuwa yakiwazunguka. Kamwe hawakuonekana kujifunza kama fungu la 19 linavyoweka wazi. “Lakini ikawa, wakati alipokufa mwamuzi huyo, wakarudi nyuma wakafanya maovu… kwa kuifuata miungu mingine…na…hawakuacha matendo yao, wala njia zao za ukaidi.” Katika sura ya 10 fungu la 6, Israeli anarudia mtindo huu wa ukaidi. Na Mungu, vivyo hivyo, bado hukiita kitendo hiki uovu.
Ibada za Baali na Ashtorethi zilijitokeza wakati wa Samweli. Samweli aliwaambia Israeli, “…iondoleeni mbali miungu migeni, nayo Maashtorethi yatoke kwenu, mkamtengenezee Bwana mioyo yenu, mkamtumikie yeye peke yake...Ndipo wana wa Israeli wakayaondoa Mabaali na Maashtorethi, wakamtumikia Bwana peke yake” (1 Sam. 7:3-4). Baadaye, katika 1 Samweli 12:10-11, Samweli aliielezea historia ya Israeli hadharani. Aliwakumbusha kwamba waliendelea kurejea katika kumtii Mungu, kisha kurudia ibada ya sanamu tena na tena!
Imesemwa kwamba “Kitu pekee ambacho mwanadamu amejifunza kutokana na historia ni kwamba hakuna mtu anayejifunza kutokana na historia.” George Santayana alienda mbele zaidi na kusema, “Wale wasiojifunza funzo la historia wana hatari ya kuirudia.”
Somo hili linawaelezea Israeli wa kale—lakini pia linaelezea ulimwengu mpya wa leo. Kwa sababu Isareli hawakudumu katika njia, hatimaye walitekwa mateka, wakapotea kutoka katika historia! Baada ya kutekwa nyara na kuadhibiwa mara moja zaidi, unabii unafunua kwamba Kristo atawakusanya kwa mara ya mwisho wakati wa Kurudi Kwake.


Mfano Mmoja wa Mwisho
Biblia husema kuwa Mfalme Sulemani alikuwa ndiye mtu mwenye hekima sana aliyewahi kuishi. Bado, alifanya kosa ambalo Mungu aliliona ni kubwa sana kiasi kwamba, baada ya kifo chake, Alimwadhibu Sulemani kwa kuuondoa ufalme kutoka kwa mtoto wake.
Kosa lake?
Alioa mwanamke aliyemwongoza katika kumwabudu Isita (Ashtorethi). Angalia 1 Wafalme 11:4-6: “Maana ikawa, Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakamgeuza moyo wake, afuate miungu mingine...Kwa kuwa Sulemani akamfuata Ashtorethi, mungu mke wa Wasidoni…Sulemani akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, wala hakumfuata Bwana kwa utimilifu, kama Daudi baba yake.” Mafungu ya 11-12 yanaonyesha kwamba ufalme ulichukuliwa kutoka kwa mtoto wake.
Makanisa Mawili: Badiliko Kubwa
Yako makanisa mawili tofauti kabisa katika Agano Jipya. Moja, ambalo ni Kanisa la kweli alilolijenga Yesu, linaelezewa kama mke wa Kristo, likiacha kujihusisha na ulimwengu huu katika desturi zake ili liwe safi bila waa lolote Anapokuja kwa ajili yake. Lakini, katika Agano Jipya lote, ilihubiriwa kuwa waalimu wa uongo watajiingiza na kushika uongozi wa ushirika wa kanisa. Wakristo wa kweli walilazimika kuzikimbia shirika zao nyingi za awali ili waendelee kumtii Mungu. Kwa namna hiyo basi, walikuwa “kundi dogo,” wakati wote wakiwa wametawanyika, kamwe hawakuwa na nguvu za kisiasa katika ulimwengu huu.
Ulimwengu umefuatilia kidogo sana nyendo za Kanisa hili dogo, lililotawanyika, lililoteswa,
lakini Kristo aliahidi kwamba hataliacha au kulisahau na kwamba “milango ya kuzimu [kaburi] haitalishinda” (Mat. 16:18).
            Japokuwa kwa vipindi lililazimika kutawanyika kwa ajili ya maisha yake (Matendo 8:1; Dan. 12:7), Kristo ametunza ahadi yake ya kubaki nalo kwa uaminifu, akiliwezesha na kulitia nguvu kwa njia ya Roho Mtakatifu.
Pamoja na mateso ya kudumu—hata vipindi vya mauaji makuu yaliyofanywa na makanisa makubwa maarufu ambayo wakati wote yametafuta kuliangamiza—kundi dogo limeendelea kusalia wakati wote kwa miaka karibu 2,000 iliyopita. Limeendelea “kushika amri za Mungu, na imani ya Yesu”  (Ufu. 14:12).
Wakati wote Mungu ameliamuru Kanisa Lake kutotunza sikukuu za kipagani! Kanisa hili dogo limehiari kumtii Mungu wakati wote. Sura nzima iliyopachikwa ya Ufunuo 12 hutoa angalizo fupi la historia yake, mpaka kipindi ambacho Mungu hulilinda muda mfupi kabla ya Kurudi kwa Kristo.
Paulo aliuonya ushirika wa Wathesalonike, “…ile siri ya kuasi hivi sasa inatenda kazi” (2 Thes. 2:7). Siri hii tayari ilishaanza kuwa na ushawishi ndani ya Kanisa la kweli miaka ishirini tu baada ya Kristo kulisimamisha katika mwaka 31 B.K. Ilikuwa ni hiyo hiyo siri ya Wakaldayo, iliyofungamanishwa katika Krismasi na Isita—sikukuu zake kubwa mbili! Mara kwa mara, kuwasili kwa sherehe hizi kuliwalazimu Wakristo wa kweli kukimbia.
Ni katika mkondo huu huu unaotenda kazi ndio umesababisha kijitabu hiki kiandikwe. Tangu kufariki kwa Herbert W. Armstrong (kiongozi wa Kanisa la Mungu kutoka mwaka 1934 hadi 1986), “ule ukengeufu” uliotabiriwa (neno la Kigiriki apostasia hapa humaanisha “kuiasi kweli”) kutokea kabla ya Kurudi kwa Kristo (2 Thes. 2:1-3) sasa ulishatokea. Maandishi mengi ya bwana Armstrong hayapo tena na yote yameandikwa upya na Kanisa la Mungu Rejeshwa.
Hivyo, shirika la Kanisa la kweli lililoelezewa hapo kabla liliungana na lile kanisa lingine, lililoonyeshwa kama malkia kahaba (kama Semiramisi/Isita) akimpanda mnyama mwenye vichwa saba (Ufu. 17). Vichwa hivi huwakilisha historia ya kuibuka kwa Himaya Takatifu ya Kirumi. Mwanamke huyu kahaba ni alama ya kanisa lenye nguvu lililojijenga kisiasa. Taratibu, kanisa hili, likiwa na makao yake makuu Roma, lilichukua na kutendea kazi mafundisho ya kipagani zaidi na zaidi hadi kufikia wakati ambapo tofauti yake na dini ya kipagani ikawa ni matumizi yake ya jina la Yesu Kristo. Hivi ndivyo Isita ilivyoanza kusherehekewa mahali pa Pasaka ya kweli ya Kikristo.

Hili “kanisa mama” lina “mabinti madhehebu” wengi, na mfumo mzima hujificha chini ya bendera ya “Ukristo”, wakati kwa hakika ni “Dini ya Kisiri ya Kibabeli.” Biblia humwonyesha kama mdanganyifu wa watu wote pamoja na nchi zote za Kikristo zikiwa zimeleweshwa na mafundisho yake ya uongo! Anaonyeshwa kama aliyelewa kwa damu ya watakatifu, wakati huo huo, akijidai kwamba yeye ndiye kanisa la kweli. Mambinti zake wote wamerithi matendo yake ya kipagani.

No comments:

Post a Comment